Psalms 41

Maombi Ya Mtu Mgonjwa

(Kwa Mwimbishaji: Zaburi Ya Daudi)


1 aHeri mtu yule anayemjali mnyonge,
Bwana atamwokoa wakati wa shida.

2 b Bwana atamlinda na kuyahifadhi maisha yake,
atambariki katika nchi
na hatamwacha katika tamaa ya adui zake.

3 c Bwana atamtegemeza awapo mgonjwa kitandani,
atamwinua kutoka kitandani mwake.


4 dNilisema, “Ee Bwana nihurumie,
niponye, maana nimekutenda dhambi wewe.”

5 eAdui zangu wanasema kwa hila,
“Lini atakufa, na jina lake litokomee kabisa.”

6 fKila anapokuja mtu kunitazama,
huzungumza uongo,
huku moyo wake hukusanya masingizio;
kisha huondoka na kuyasambaza huku na huko.


7 gAdui zangu wote hunong’onezana dhidi yangu,
hao huniwazia mabaya sana, wakisema,

8 h“Ugonjwa mbaya sana umempata,
kamwe hatainuka tena kitandani mwake.”

9 iHata rafiki yangu wa karibu niliyemwamini,
yule aliyekula chakula changu
ameniinulia kisigino chake.


10 jLakini wewe, Ee Bwana, nihurumie,
ukaniinue tena, ili niweze kuwalipiza kisasi.

11 kNajua kwamba wapendezwa nami,
kwa kuwa adui yangu hanishindi.

12 lKatika uadilifu wangu unanitegemeza
na kuniweka kwenye uwepo wako milele.


13 mMsifuni Bwana, Mungu wa Israeli,
tangu milele na hata milele.
Amen na Amen.
Copyright information for SwhKC